KIUNGO Mtanzania Diana Msewa anayechezea klabu ya Trabzonspor ni miongoni mwa wachezaji waliomaliza Ligi Kuu ya Uturuki (W) na rekodi nzuri kwenye mechi 14 alizocheza.
Septemba 20 mwaka jana Msewa alitambulishwa kwenye kikosi cha Trabzonspor ya Wanawake akitokea Amed SK ya nchini humo.
Nyota huyo wa timu ya taifa ya wanawake, Twiga Stars, kwenye mechi 14 alizocheza amefunga mabao manane na kutoa asisti saba.
Licha ya kucheza kwenye eneo la kiungo lakini amekuwa na msaada mkubwa kwenye kikosi hicho akisaidia kwenye kuzuia na kuipatia timu hiyo mabao.
Msewa amefikia rekodi yake ya msimu uliopita akiwa na Amed S.K ambayo ndani ya msimu mzima alifunga mabao manane na kutoa asisti tano.
Kiungo huyo amekuwa mhimili mkubwa kwenye kikosi hicho kilichomaliza msimu kikiwa nafasi ya tano kwenye msimamo wa ligi kikikusanya pointi 48.
Taarifa za michezo nchini Uturuki zinaeleza kuwa Trabzonspor inamuandalia ofa nono Msewa, ili aweze kuendelea nayo msimu ujao kwani alisaini mkataba wa mwaka mmoja na sababu ya kufanya hivyo ni baada ya kuonyesha kiwango bora.